THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

INFORMATION AND COMMUNICATION TECHNOLOGIES COMMISSION

Viongozi wa Taasisi za TEHAMA waweka Mikakati ya kupaisha TEHAMA Nchini

  • News

TUME ya Tehama nchini (ICTC) na viongozi wa Taasisi za Tehama wamekutana jijini Arusha ili kuweka mikakati ya kuendelea kuleta mageuzi makubwa katika ukuzaji wa teknolojia ya habari na mawasiliano.

Akizungumza jijini humo kwenye mafunzo ya kuwajengea uwezo Makamishna wa Tume hiyo na viongozi wa Taasisi za Tehama,Mkurugenzi Mkuu wa ICTC, Dk. Nkundwe Mwasaga, amesema wameamua kutoa mafunzo maalumu na kujadiliana ni namna gani nchi nyingine duniani zinafanya ili kuongoza taasisi zao na wanatumia nyenzo gani kuendesha taasisi zao.

“Tume ina majukumu makuu mawili, kwanza ni kuratibu utekelezaji wa Sera ya Tehama ya Taifa na jukumu la pili ni kukuza Tehama. Hivyo, tumekuja kwa ajili ya mafunzo mbalimbali Arusha, na tuna wawezeshaji kutoka Taasisi ya Uongozi na Ofisi ya Hazina nchini. Kimsingi, tunatarajia kupata uelewa wa kutosha kuhusu mipaka ya Makamishna wa Tume, Uongozi wa Taasisi,”amesema.

Naye, Kamishna wa bodi ya Tume ya TEHAMA ambaye pia ni Profesa wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), Prof. George Oreku, ameshauri serikali iweke msukumo mkubwa kwenye kampuni za Tehama, hususani kampuni za vijana kutokana na fursa nyingi zinazotokana na mabadiliko ya TEHAMA. Hicho kitapelekea utengenezaji wa kazi kwa vijana na kuongezeka pato la taifa linaloyokana na shughuli zinazotumia TEHAMA.

Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk. Faisal Issa ambaye pia ni Kamishna wa Tume ya TEHAMA, amesema mafunzo hayo yatawajenga kwa kuwapa upeo wa kutenda vyema katika majukumu yao.